Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

ZINGATIENI MAADILI UTU NA HESHIMA KATIKA KUTOA HUDUMA ZA AFYA.

Posted on: January 10th, 2024



Na: WAF, Dodoma.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Grace Magembe amewataka wahudumu wa afya kuzingatia utoaji wa huduma bora kwa wananchi kupitia misingi ya maadili, utu na heshima ili kuendelea kuleta mabadiliko na maendeleo yanayoendana na utoaji wa huduma.


Dkt. Magembe amesema hayo Januari 10, 2024 wakati akifungua kikao kazi cha kada za Madaktari na wauguzi kilichofanyika Mkoani Dodoma chenye lengo la kujadili namna ya kuboresha utoaji huduma bora wananchi.


Dkt. Magembe amesema utoaji wa huduma bora kwa wananchi utasaidia kuleta upendo na heshima hivyo kusababisha wananchi kufurahia huduma zinazotolewa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya nchini.


“Ndani ya miaka miwili ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewezesha upatikanaji wa huduma za Afya karibu na wananchi kwa asilimia 70 kwa mijini na vijijini hivyo wananchi wanafikiwa na huduma za afya ndani ya km 5, hatuna tunachomdai Rais Maendeleo na mafanikio kwenye Sekta ya Afya ni makubwa kinachotakiwa sasa hivi ni sisi watumishi kubadilisha fikra zetu na uwajibikaji wetu”. Amesema Dkt. Magembe.


Aidha, Dkt. Magembe amesema hakuna huduma bora bila mabadiliko ya watumishi katika kila kada ndani ya sekta ya afya hivyo ni lazima kuangalia kwa uhalisia kwani suala la kuhudumia wananchi kwa heshima, haki linaanzia getini wakati mgonjwa anaingia kufuata huduma.


Dkt. Magembe amewashukuru wadau wa maendeleo katika sekta ya afya kwa kushirikiana na Serikali na kuhakikisha wanafikisha huduma kwa makundi yote ya Wananchi.


Mwisho, Dkt. Magembe amewahakikishia watanzania kutokanana na maboresho yote yaliyofanyika katika Sekta ya Afya muelekeo wa serikali ni kujikita zaidi kwenye ubora wa utoaji huduma ili ziendane na maboresho haya.