WAMILIKI VITUO VYA TIBA ASILI, TIBA MBADALA WATAKIWA KUSAJILIWA
Posted on: March 19th, 2025
Na WAF - Dodoma
Wamiliki wa vituo vinavyotoa huduma ya tiba asili na tiba mbadala nchini wametakiwa kuhakikisha vituo hivyo vinasajiliwa kisheria na kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa na Serikali.
Hayo yamesemwa Machi 18, 2025 jijini Dodoma na Mfamasia wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala Bw. Ndahani Msigwa kwa niaba ya Msajili wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala Bw. Martin Magogwa wakati wa zoezi la ukaguzi shirikishi wa vituo vya kutolea huduma hizo linaloendelea nchini.
Bw. Msigwa amesema lengo la zoezi hilo ni kukagua ubora wa huduma, vituo na kujiridhisha kama vimesajaliwa, vinafuata kanuni na miongozo ya baraza hilo kwa mujibu wa Sheria ya Tiba Asili na Tiba Mbadala Na. 23 ya Mwaka 2002.
Bw. Msigwa amesema kwa upande wa watoa huduma nao wanatakiwa kuhakikisha wanasajiliwa na baraza na kusisitiza kuwa watoe huduma kwa kuzingatia wigo wa huduma kwa mujibu wa leseni walizopatiwa kisheria.
Ameongeza kuwa kwa sasa zoezi linaloendelea ni shirikishi lakini baadae hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa watakaokaidi taratibu za kisheria.
Kwa upande wa utoaji huduma na matumizi ya vifaa ambavyo haviruhusiwi Bw. Msigwa amewaasa watoa huduma za tiba asili wanaotumia nyara za serikali na vifaa visivyoruhusiwa kuacha mara moja.
“Mfano wa vifaa hivyo ni ‘Quantum Resonance Magnetic Analyzer’,vifaa hivyo vilishakatwazwa na Serikali kutumika katika upimaji wa afya, hivyo vimechukuliwa wakati wa ukaguzi, pia Serikali imepiga marufuku uuzaji wa dawa aina ya mkongo na akayabagu,” amesema Bw. Msigwa
Bw. Msigwa amewaelekeza viongozi wote walio katika ngazi za mikoa na halmashauri kuhakikisha wanafanya ukaguzi mara kwa mara wa kliniki bubu zilizofunguliwa kwa mgongo wa tiba asili na tiba mbadala na kutoa tiba kwa kutumia vyakula (food products) kinyume na Sheria.
“Kumekuwa na wimbi la watu wanaofungua kliniki na kutibu wagonjwa kupitia vyakula au tiba lishe.