Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

SERIKALI KUANZISHA TAASISI MPYA ITAKAYO TOA HUDUMA ZA UPASUAJI WA UBONGO NA MISHIPA

Posted on: April 27th, 2024


Na WAF – Dar Es Salaam 


Serikali kupitia Wizara ya Afya imedhamiria kuanzisha Taasisi mahususi ambayo itakuwa inashuhulikia masuala ya upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu ili iweze kuboresha zaidi huduma hizo za ubingwa kuitoa katika Taasisi ya Mifupa Ubongo (MOI) ambapo itabakia na masuala ya upasuaji wa mifupa pekee. 


Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema hayo leo Aprili 27, 2024 baada ya uzinduzi wa chama cha madaktari bingwa wa ubongo na mishipa ya fahamu (Tanzania Neurosurgical Society) kikiongozwa na Rais wa chama hicho Dkt. Othmani Kiloloma Jijini Dar Es Salaam.


“lengo la chama hichi ni kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora na salama za upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu, ikiwemo upatikanaji wa madaktari bingwa wa upasuaji ubongo na mishipa ya fahamu”. Amesema Waziri Ummy


Amesema, Tanzania kuna madaktari bingwa wa upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu 25 tu, ambapo kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) inapendekeza angalau katika kila watu 150,000 kuwe na daktari bigwa wa upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu Mmoja.


“Ukichukua idadi ya madaktari bigwa wa upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu 25 tulionao maana yake kwa Tanzania daktari bigwa Mmoja anahudumia Watanzania Mil 2,400,000, huduma hizi bado hazijawafikia Waanzania wengi ndio maana chama hichi kimekuja ili pia kujengeana uwezo na kuhamasisha madaktari wengine waweze kusomea fani hiyo ya upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu”. Amesema Waziri Ummy


Aidha, Waziri Ummy amesema, Serikali inaendelea kuboresha huduma za Afya ikiwemo kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za kibingwa, usambazaji wa maafisa wa Afya katika vituo vyote vya Afya na Hospitali, uanzishwaji wa huduma za kina za upasuaji katika Hospitali za Rufaa za Kanda na ukuzaji wa wataalamu wadogo katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. 


“Lakini pia Serikali imeendelea kuweka msisitizo wa elimu endelevu katika taaluma za upasuaji ikiwa ni pamoja na upasuaji wa Neurosurgery, Neuro-radiology, Neuropathology, Neuro-anesthesiology, critical care, Neurology, pamoja na Neuro-rehabilitation”. Amesema Waziri Ummy 


Pia, Waziri Ummy amesema Serikali imeendelea kuimarishwa upatikanaji mkubwa wa huduma za uchunguzi kupitia CT-scan katika Hospitali zote za Rufaa za Kanda pamoja na ujumuishaji wa huduma za MRI na huduma za ‘Angiography’ katika vituo vya ngazi ya juu ili kumrahishia Mtanzania kupata huduma hizo za uchunguzi ndani ya nchi.