Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

JAPAN NA VODACOM KUENDELEA KUIMARISHA SEKTA YA AFYA NCHINI.

Posted on: April 18th, 2023

Na. WAF - Dar Es Salaam

Serikali ya Japan imetoa majokofu mia tatu tisini (390) ya kuhifadhia chanjo kwa Serikali ya Tanzania pia Kampuni ya Vodacom imetoa vyumba vya baridi (cold rooms) Sita pamoja na ukarabati wa majengo ya Mpango wa Taifa wa Chanjo.

Misaada hiyo imetolewa leo na kupokelewa na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu kwa niaba ya Serikali katika ofisi za Mpango wa Taifa wa Chanjo jijini Dar es Salaam.

“Serikali inathamini sana misaada ya wadau wa maendeleo inayotolewa kwa ajili ya Sekta ya Afya, Wizara itahakikisha inasimamia ipasavyo misaada hii kwa kuvitunza vyumba hivyo Sita vya ubaridi na majokofu haya ambayo yatatumika kutunzia chanjo katika ngazi ya mikoa, halmashauri na vituo vya kutolea huduma,” amesema Waziri Ummy

Waziri Ummy ametoa rai kwa watoa huduma kutunza majokofu haya pamoja na vyumba hivyo vya baridi ili lengo lililokusudiwa liweze kufikiwa na wananchi waweze kupata huduma ya chanjo iliyo bora ili kukabiliana na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Aidha, Waziri Ummy amesema lengo la Serikali ni kuimarisha huduma za afya ikiwemo utoaji wa huduma ya chanjo kwa watoto wenye uhitaji ambapo majokofu yaliyotolewa pamoja na vyumba vya baridi (Cold Rooms) yataboresha ubora wa kuhifadhi chanjo katika mnyororo baridi kwenye Mikoa ya Arusha, Dar es salaam, Lindi, Mtwara, Shinyanga, Simiyu, Singida, Dodoma, Katavi, Rukwa, Tabora, Kigoma, Songwe, na Zanzibar ambapo majokofu haya yatafungwa.

“Natambua kuwa Nchi yetu bado inauhitaji mkubwa wa majokofu ya kuhifadhia chanjo, lengo la Serikali ni kuwa na majokofu ya kisasa ambayo yameunganishwa na vifaa maalumu vya kupima joto la hali ya chanjo na kutuma taarifa kwa wahusika hata wanapokuwa mbali na kituo cha kuhifadhia,” amesema Waziri Ummy

Ili kufanikisha azma hiyo Waziri Ummy amebainisha kuwa jumla ya majokofu 5,822 yanahitajika kufungwa katika vituo vya kuhifadhia chanjo hapa nchini ambapo hadi sasa Serikali imenunua jumla ya majokofu mapya 2,012 kati ya 5,822 yanayohitajika.

Hata hivyo, ununuzi wa majokufu 3,810 yaliyosalia yanaendelea kwa kushirikiana na shirika la UNICEF ili kutimiza azma ya Serikali kuwa na majokofu 5,822.