Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

WADAU WATAKIWA KUZINGATIA TAKWIMU SAHIHI KWENYE MAPAMBANO DHIDI YA SARATANI

Posted on: May 22nd, 2025

Na WAF, Dodoma 


Kamati ya Ushauri ya Usajili wa Saratani (ACCR) imetoa wito kwa  wadau mbalimbali kuwa na mapango madhubuti wa kuwa na takwimu sahihi ili kusaidia Serikali kuweka sera na mikakati sahihi ya kupambana na saratani nchini.

 

Wito huo umetolewa leo Mei 22, 2025 Jijini Dodoma na mmoja wa wajumbe wa Kamati hiyo ambaye pia ni Meneja Mpango wa Magonjwa yasiyo ya kuambukiza kutoka Wizara ya Afya, Bi. Edith Bakari wakati wa kuhitimisha kikao cha pili baada ya kamati hiyo kuzinduliwa jana jijini hapa.


 Bi Edith amesema kamati hiyo itadumu kwa miaka mitatu na itakuwa ikitoa ushauri kwenye masuala ya saratani.


Amesema kamati ina lengo la kukusanya takwimu sahihi za ugonjwa wa saratani ambazo zitasaidia Taifa  kupambana na ugonjwa huo kwa ufasaha .


“Kamati zetu hizi tulivyozitengeneza hii itakuwa  ni  kamati kuu na katika kila kamati kuu kutakuwa na kituo ambacho kitakuwa kinafanya usajili na wa kamati ndogo ambayo itaunganisha vituo vyote vinavyotoa huduma pamoja na wadau bila kusahau wagonjwa ,” ameeleza Bi. Edith.


Amesema kamati kuu pia imejumuisha wagonjwa ili waweze kusikia sauti ya kila mdau na kuwasaidia kuweka mipango sawa ambapo kamati ya vituo itakuwa ikiripoti kwa kamati kuu ili  kuchukua takwimu kwa  kamati ya  kitaifa. 


Kwa upande wake  mjumbe Dkt. Julius Aloyce kutoka Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini, KCMC, amesema   ugonjwa wa saratani unakuwa kwa kasi katika jamii, hivyo lazima kuwe na takwimu sahihi za  kuisaidia Serikali kuweka mipago madhubuti ya kupambana na saratani.


“Ni wakati sahihi wa kuona ni namna gani tunaweza kuongeza ufanisi katika magonjwa ya saratani na jinsi ya kuboresha katika jamii ya watanzania,” amesema Mtaalam huyo.


Hata hivyo ametoa wito  kwa Watanzania kuwa na utayari  wa kujifunza na kupambana na saratani kwa kuhakikisha zinapatikana takwimu sahihi na kwa wakati.


“Kuna sintofahamu  mtu anapojulikana ana   saratani hii inachagizwa kwa kutokuwa na uelewa kuwa ni janga kubwa hivyo kila mmoja yupo hatarini, hivyo ni jukumu letu kujifunza jinsi ya kuepuka  na saratani pamoja  na kufanya uchunguzi na hatua  zipi  za kufuata kwa usahihi,” amesema Dkt. Aloyce.