Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

UPATIKANAJI WA DAWA UMEONGEZEKA KUFIKIA ASILIMIA 79 MWAKA 2023/24

Posted on: May 14th, 2024

UTEKELEZAJI WA BAJETI YA WIZARA YA AFYA 2023/24


Na WAF - Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya imebainisha kuwa katika kipindi cha Mwaka 2023/24 upatikanaji wa bidhaa za Afya umeongezeka hadi kufikia asilimia 79 kutoka wastani wa asilimia 73 Mwaka 2022/23.

Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu amesema hayo Bungeni Mei 13, 2024 akiwa anawasilisha hotuba yake ya bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2024/25 akielezea utekelezaji wa majukumu ya Wizara katika utoaji wa huduma za Kinga nchini.

"Upatikanaji wa bidhaa za Afya kutokana na utekelezaji wa bajeti ya Mwaka 2023/24 Zahanati ni asilimia 69, Vituo vya Afya asilimia 66, Hospitali za Wilaya asilimia 72, Hospitali za Rufaa za Mikoa asilimia 94, Hospitali za Kanda, Maalum na Taifa ni asilimia 89." Amesema Waziri Ummy

Aidha, Waziri @ummymwalimu amesema kwa Mwaka 2023/24, Serikali imepeleka Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kiasi cha Shilingi Bilioni 103,333,333,343.67 sawa na asilimia 50.3 ya Bajeti ya Shilingi Bilioni 205 iliyoidhinishwa kwa ajili ya ugharamiaji wa mnyororo mzima wa upatikanaji wa bidhaa za afya.

"Pia, Vituo vya kutolea huduma za afya kupitia fedha za uchangiaji vimepeleka MSD kiasi cha Shilingi Biliini 57,528,128,119.49 kwa Mwaka 2023/24, vilevile Serikali imetoa jumla ya Shilingi Bilioni 100,000,000,000 ikiwa ni sehemu ya mtaji ulioombwa na MSD kwa ajili ya kuimarisha upatikanaji wa dawa nchini." Amesema Waziri Ummy