Customer Feedback Centre

Ministry of Health

HOSPITALI ZA MIKOA ZATAKIWA KUFIKIA LENGO LA UKUSANYAJI DAMU KWA ASILIMIA 85 HADI 90

Posted on: October 3rd, 2023


Na Mwandishi Wetu-Dodoma


KATIKA juhudi za kutatua changamoto ya uhitaji wa damu Salama nchini,Serikali imeziagiza hospitali za Mikoa kufikia lengo la kukusanya damu kwa asilimia 85 hadi 90.


Hayo yameelezwa leo Oktoba 3, 2023 Jijini Dodoma na Kaimu Katibu Mkuu kutoka Wizara ya Afya,Bi.Ziada Sellah wakati akizindua zoezi la uchangiaji damu kwa wajumbe wa baraza la mashirika yasiyo ya kiserikali (NACONGO) kuelekea Mkutano Mkuu wa Mashirika hayo.


Bi.Ziada amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika zoezi la uchangiaji wa damu kwani itaokoa maisha ya wengi wenye uhitaji hususani wagonjwa mahututi.


“Natoa rai watu wajitokeze kwa wingi katika zoezi hili la kuchangia damu kwani wagonjwa wanapozidiwa na kuhitaji damu ni lazima wapatiwe kwa uharaka ,Kina Mama wanapoenda kujifungua wanakua katika hatihati ya kupoteza damu nyingi na uhitaji wa damu unatakiwa uwe wa papo hapo bila mjadala ili kunusuru maisha yao”amesema Bi.Ziada.


Aidha ameupongeza Mkoa wa Dodoma kwa kuvuka lengo la kukusanya damu kwa asilimia 110 na kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kuokoa maisha kwa watu wenye uhitaji wa damu.


"Tunajua kuwa hakuna kiwanda cha kutengeneza damu wala haiuzwi hivyo niwaombe wananchi wajitokeze kwa wingi kuchangia damu ili tuokoe maisha kwa sababu ukichangia chupa moja unaokoa maisha ya watu wawili ya mama na mtoto," amesema Bi.Ziada.


Hata hivyo amesema kuwa bado kuna Mikoa ambayo ipo chini kwenye uchangiaji damu ambayo inakusanya kwa asilimia 20 hali inayoonyesha kuwa ina uwezo wa kuokoa maisha ya watu wenye uhitaji wa damu kwa asilimia 20 huku asilimia 80 ikikosa huduma hiyo.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali Mhe.Mwantumu Mahiza amesema pamoja na kukutana kwa ajili ya mkutano wa baraza lakini wamejipanga kufanya shughuli zingine za kijamii kama vile kupanda miti, kuchangia damu na kutembelea kituo cha watoto yatima lengo likiwa ni kurudisha fadhila kwa jamii inayowazunguka.


“Kuchangia damu ni sadaka nzuri sana kwani ni suala linaloenda kunusuru maisha ya mtu anaepigania maisha yake hivyo nawasisitiza wananchi kujitokeza kwa wingi na Mwenyezi Mungu atatubariki”amesema Mhe. Mwantuma.


Awali Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Nelson Bukuru ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kuchangia damu kwenye kituo cha damu salama cha Kanda ya kati pamoja na kituo cha afya cha Makole ambapo huduma hiyo ipo kila siku za kazi kwa ajili ya kuokoa maisha


“Wananchi wengi hawajui kwamba zoezi la kuchangia damu linaweza kufanyika siku yeyote mtu anapoamua kuchangia kwani anaweza kwenda hospitali na kuchangia na si suala la mara moja,anaweza kuchangia mara nyingi awezavyo endapo ana vigezo vya kuchangia damu”amesema Dkt.Bukuru