Customer Feedback Centre

Ministry of Health

WAWEKEZAJI WA DAWA NA VIFAA TIBA KUTOKA INDIA WAVUTIWA KUWEKEZA TANZANIA

Posted on: July 28th, 2023

Wawekezaji wa bidhaa za dawa na vifaa tiba kutoka India wavutiwa kuwekeza Tanzania ambayo pia ni mlango wa sahihi wa kulifika soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa jangwa la Sahara lenye idadi ya watu zaidi ya Milioni 745.

Hayo yamesemwa na Waziri Ummy Mwalimu Julai 27, 2023 mara baada ya kufanya kikao na wafanyabiashara ambao wamewekeza katika sekta ya dawa na vifaa tiba nchini Tanzania kikao kilichoandaliwa na shirikisho la wenye viwanda la nchini India yaani Federation of India Chambers of Commerce and Industry. ( FICCI) Jijini New Delhi India.

“Tanzania inategemea na kuagiza zaidi ya asilimia 60 ya dawa na vifaa tiba kutoka nchini India. Hivyo kupitia kikao hiki, tumewahakikishia kuwa Serikali itatoa ushirikiano mkubwa kwa wafanyabiashara hawa pindi wanapotakiwa kuzingatia taratibu za ukaguzi, usajili na uingizaji wa dawa na vifaa tiba na kufanya uwekezaji nchini Tanzania” amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amebainisha kuwa kwenye ziara yake hiyo ameambatana na Wataalam kutoka TMDA pamoja na Mfamasia Mkuu wa Serikali ambapo kwa pamoja wametoa ufafanuzi wa hoja zilizoibuliwa na wafanyabiashara hao jambo ambalo liliwafurahisha na kuwaongezea ari ya kufanya uwekezaji nchini Tanzania.

Hata hivyo Waziri Ummy ametumia fursa hiyo kutangaza vivutio vya utalii wa Tanzania na kuwahamasisha wafanyabishara hao kutembelea Tanzania kwa shughuli za utalii huku wafanyabiashara hao wakiomba Serikali kutangaza zaidi vivutio hivyo kupitia Ubalozi wa Tanzania mjini New Delhi tayari waneanza taratibu za kutangaza vivutio hivyo ambapo watashirikiana na Wizara ya Utalii katika kuhakikisha kuwa vivutio vyote vya utalii vinatangazwa ikiwa ni pamoja na taratibu zote za kufanya utalii.