Customer Feedback Centre

Ministry of Health

VIFAA TIBA VYA HUDUMA KWA WATOTO WACHANGA VYAANZA KUSAMBAZWA NCHINI

Posted on: July 16th, 2023

Na. WAF - Shinyanga

Vifaa tiba kwa ajili ya huduma za watoto wachanga wagonjwa na njiti vyenye thamani ya Tsh.Bilion 6.3 vimeanza kusambazwa kwenye Hospitali mbalimbali Nchini.

Waziri wa Afya Mhe. ummy mwalimu amebainisha hayo wakati akihitimisha ziara yake ya kukagua huduma za Afya pamoja upatikanaji wa dawa Mkoa wa Shinyanga.

“Wizara ya Afya kwa kutumia fedha za IMF za ahueni ya UVIKO-19, imenunua vifaa tiba kwa ajili ya huduma za watoto wachanga vyenye thamani ya Tsh.Bilion 6.3 kupitia Bohari ya Dawa ambavyo vimeanza kusambazwa kwenye Hospitali mbalimbali nchini”, amesema Waziri Ummy

Aidha, Waziri Ummy amesema vifaa hivyo vimeanza kusambazwa kwenye Hospitali 123 katika Halmashauri 119 kutoka Mikoa yote nchini ambavyo vitakwenda kusaidia huduma za watoto wachanga wagonjwa na watoto njiti.

“Hospitali hizi ni zile zilizotoa taarifa ya kuwa zimeanzisha wodi maalum kwa ajili ya matibabu ya Watoto wachanga wagonjwa na watoto waliozaliwa kabla ya muda (njiti) “Neonatal Care Units (NCUs)”, amesema Waziri Ummy

Amesema, Katika Mkoa wa Shinyanga Hospitali Tatu zinazonufaika na mgao huo ni Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kahama imepangiwa vifaa vya thamani ya Tshs Mil. 64, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga imepangiwa vifaa vya thamani ya Tshs Mil. 65, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu (Jakaya Kikwete Hospital) imepangiwa vifaa vya thamani ya Tshs Mil. 40.

Katika hatua hiyo, Waziri Ummy amezitaka Hospitali zote za Halmashauri nchini kuwepo na huduma za uangalizi Maalum kwa Watoto Wachanga (NICU).

Waziri Ummy alitoa agizo hilo Julai 13, 2023 alipokuwa anaongea na timu ya usimamizi wa Afya ya Mkoa, Wataalam wa Afya ngazi ya Jamii pamoja na Madaktari Bingwa katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Shinyanga.

“Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshafanya jukumu lake la kutoa fedha hizo Sasa ni jukumu letu kuimarisha huduma za watoto wachanga ili mama mjamzito akienda kujifungua basi inapendeza sana atoke na mtoto wake”, amesema Waziri Ummy

Waziri Ummy ameongeza kusema kuwa, hata mtoto akizaliwa na gram 500 anapaswa kuishi.