Customer Feedback Centre

Ministry of Health

US - CDC YAAHIDI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA TANZANIA KATIKA KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA

Posted on: September 27th, 2023

Na. WAF - Atlanta, Marekani


Taasisi ya kukinga na kudhibiti Magonjwa ya Marekani (US - CDC) imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuimarisha huduma za Afya ya Jamii.


Hayo yamebainishwa Jana Septemba 26, 2023 na Mkurugenzi wa masuala ya Afya ya kimataifa wa US - CDC Dkt. Howard Zucker wakati wa ziara ya Waziri wa Afya Tanzaniza Mhe. @ummymwalimu (Mb) na Waziri wa Afya wa Zanzibar Mhe. Nassor Mazrui (Mb) walipoitembelea Taasisi hiyo.


Aidha, Waziri Ummy amesema yeye pamoja na Waziri Mazrui na timu waliyoambatana nayo wametembekea Taasisi hiyo kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika uendeshaji wa mifumo ya kuzuia na kukabiliana na magonjwa katika jamii pamoja na kujifunza uundwaji na uendeshaji wa Taasisi ya Taifa ya Afya ya Jamii.


“Tumefanya mazungumzo na viongozi wa juu wa Taasisi hii ya US - CDC wakiongozwa na Mkurugenzi wa masuala ya Afya ya Kimataifa wa US - CDC Dkt. Howard Zucker ambapo ameipongeza sana Serikali ya Tanzania kwa uongozi imara katika kuboresha huduma za Afya ya jamii”. Amesema Waziri Ummy


Pia, Taasisi ya US - CDC imetoa tuzo za kutambua michango ya Mhe. Ummy na Mhe. Mazrui katika kutambua usimamizi thabiti na wenye matokeo katika kudhibiti janga la UVIKO - 19.


Sambamba na hilo, Waziri Ummy alimshukuru Mkurugenzi Mkazi wa CDC nchini Tanzania Dkt. Mahesh Swaminathan kwa kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa vipaumbele vya Serikali hususani katika kupambana na magonjwa ya UKIMWI na Kifua Kikuu pamoja na masuala ya usalama wa Afya ya Kimataifa.


“Lakini pia naishukuru na kuipongeza sana US - CDC kwa kutoa msaada wa kitaalam na rasilimali fedha zilizowezesha kudhibiti ugonjwa wa Virusi vya Marburg uliotokea nchini Tanzania na kufanikiwa kuumaliza mlipuko huo ndani ya muda mfupi”. Amesema Waziri Ummy


Viongozi hao walikubaliana kuendelea kushirikiana katika kuimarisha uratibu wa magonjwa ya Afya ya jamii na kukabiliana na magonjwa ya milipuko ambapo US - CDC waliahidi kutoa msaada wa kitaalam na rasilimali fedha zitakazowezesha kuanzisha Taasisi ya Taifa ya Afya ya Jamii nchini Tanzania.