Customer Feedback Centre

Ministry of Health

PUNGUZENI SEMINA, WANANCHI WAPATE HUDUMA VITUONI

Posted on: July 9th, 2023

Na. WAF - Bariadi, Simiyu

Waziri wa Afya, Mhe Ummy Mwalimu amewataka wataalamu wa afya nchini kupunguza semina ili kuwa na muda zaidi wa kutoa huduma bora za matibabu kwa wananchi.

Waziri Ummy Mwalimu ameyasema hayo leo Julai 10, 2023 katika ziara yake Mkoani Simiyu wakati akizungumza na Viongozi wa Mkoa huo na Menejimenti ya Afya ya Mkoa chini ya Mkuu wa Mkoa Dkt. Yahaya Nawanda.

“Wataalamu wa afya punguzeni semina maana mmekuwa na semina nyingi hadi kupelekea wagonjwa kukosa huduma kwa wakati na kumekuwa na msomgamano mkubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya sababu ya semina”, amesema Waziri Ummy Mwalimu

Aidha, Waziri Ummy Mwalimu amesema kuwa katika utolewaji wa huduma za afya nchini hakuna kilichosimama kwakuwa Serikali imejenga majengo ya hospitali, imetoa dawa na vifaa tiba, hivyo ni jukumu la wataalamu wa Afya kutoa huduma bora patika vituo hivyo.

“Tunamshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia kila kitu katika Sekta ya Afya ikiwemo majengo, vifaa tiba, kuajiri wataalamu na sasa ni jukumu letu wataalamu kutoa huduma bora kwa wananchi kwani ndio dhamira ya Serikali”, amesema @ummymwalimu

Pia, Waziri @ummymwalimu ameutaka uongozi wa Mkoa wa Simiyu kuwasimamia madaktari ili wafanye kazi kwa weledi kwa kuangalia historia ya mgonjwa ili apate huduma sahihi na kwa wakati.

Ameongeza kuwa, lengo la Serikali ni kutoa huduma bora za Afya kwa Watanzania na kwa mara ya kwanza Serikali imetoa hela za dawa kwa asilimia 100, hivyo amevitaka vituo vyote vya Afya kuwa na Dawa zote muhimu ili kumsaidia mwananchi kupata huduma za matibabu kwa wakati.

Hata hivyo, Waziri Ummy ametoa rai kwa watoa huduma nchini kuzingatia utumiaji wa lugha nzuri, weledi na maadili na kuzingatia viapo vya wataalam wa afya wakati wa kuwahudumia wananchi.