Customer Feedback Centre

Ministry of Health

MAAMBUKIZI YA VIRUSI VYA UKIMWI YAMEPUNGUA KUFIKIA ASILIMIA 1.7 MKOA WA LINDI

Posted on: February 29th, 2024



Na. WAF - Lindi

Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI yamepungua katika Manispaa ya Mkoa wa Lindi kutoka asilimia 2 hadi asilimia 1.7 Mwaka 2023 ambayo imepelekea kufikia malengo ya 95-95-95 katika Mkoa huo huku viongozi wa Mkoa huo wametakiwa kutobweta waendelee kuchukua hatua kwa kutoa elimu.

Wazir Ummy Mwalimu amesema hayo jana Februari 29, 2024 akiwa katika ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Lindi baada ya kutembelea katika kituo cha Afya Mnazimmoja, kituo cha Afya cha Mjini, Zahanati ya Nachingwea pamoja na kutembelea Chuo cha Afya na Sayansi Shirikishi.

“Niwapongeze Mkoa wa Lindi Mmefikia malengo ya 95-95-95 ambapo asilimia 96 ya watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI wanajua kwamba wana maambukisi ya UKIMWI, asilimia 95 ya watu wenye maambukizi wapo kwenye dawa na katika asilimia hiyo 95 ya wanaotumia dawa Virusi vimefubazwa.” Amesema Waziri Ummy

Aidha, Waziri Ummy amewataka wananchi kuzingatia mtindo bora wa maisha ikiwemo kufanya mazoezi, ulaji wa vyakula kwa kupungua chumvi nyingi, sukari nyingi na mafuta mengi ili kuepuka kupata magonjwa Yasiyoambukiza ikiwemo Kisukari.

“Miaka Mitano iliyopita huwezi kuona Kisukari, huwezi kuona shinikizo la juu la damu kwenye magonjwa matano yanayowasumbua Watanzania wengi.” Amesema Waziri Ummy

Waziri Ummy anatarajia kumaliza ziara yake ya kikazi Mkoani Lindi leo Machi 1, 2024 baada ya kutembelea katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi (Sokoine) pamoja na kuzungumza na Kamati ya Afya Ngazi ya Mkoa (RHMT)na Kamati ya Afya Ngazi ya Wilaya (CHMT)