Customer Feedback Centre

Ministry of Health

HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA IRINGA KINARA KATIKA KUBORESHA HUDUMA ZA UTENGAMAO NA TIBA MAZOEZI, MATENGENEZO YA VIFAA TIBA NA MIUNDOMBINU

Posted on: July 18th, 2023

Na. WAF, Iringa

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Grace Magembe amezitaka Hospiatali za Rufaa nchini kuhakikisha zinatoa huduma za utengamao na tiba mazoezi ili kuwezesha wananchi wenye uhitaji wakiwemo watoto wenye ulemavu kuishi maisha yenye ubora na kuweza kujihudumia wao wenyewe

Dkt. Magembe ametoa wito huo leo Mkoani Iringa katika ziara ya kikazi inayofanywa kwa pamoja na Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI Dtk.Charles Mahera kukagua utoaji na ubora wa huduma kuanzia ngazi ya msingi hadi rufaa, ambapo wamekagua hali ya utoaji Huduma katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Iringa na Hospitali ya Halmashauri ya Iringa Frelimo.

Viongozi hao walijionea namna Hospitali hiyo ilivyokuwa na karakana ya kisasa ya kutengeneza viungo bandia ikiwemo miguu, mikono na vifaa saidizi mbalimbali.
Wameweza kupata ufafanuzi kutoka kwa wataalamu waliobobea katika taaluma ya kutoa huduma za utengemao na mazoezi tiba waliopo katika Hospitali hiyo.

Pia, wameona karakana ya kisasa yenye uwezo wa kufanya matengenezo na marekebisho vifaa tiba vyote vya hospitali hiyo pamoja na Hospitali za Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati za Mkoa wa Iringa.

“Niwapongeze kwa kuwa na karakana hii kubwa na nzuri ya kutengeneza vifaa tiba na viungo bandia ambayo inasaidia Mkoa mzima ikiwemo vituo vilivyopo kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa.

"Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa fedha nyingi kununua vifaa tiba vya kisasa kuanzia ngazi ya msingi hadi taifa, ni lazima tuwe na mpango wa matengenezo, ili vikiharibika kidogo visiwekwe stoo kwani itakuwa ni hasara kwa serikali na kuwanyima wananchi huduma”, amesisitiza Dkt. Grace.