Customer Feedback Centre

Ministry of Health

BUNGE LAPITISHA AZIMIO LA MAPENDEKEZO YA KURIDHIA MKATABA WA KUANZISHA TAASISI YA DAWA YA AFRIKA YA 2019

Posted on: October 31st, 2023


Na. WAF


Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 31, Oktoba 2023, limepitisha azimio la Mapendekezo ya Kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika ya Mwaka 2019 (Treaty for Establishiment of the African Medicines Agency -AMA ) katika bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo Jijini Dodoma wakati wa Bunge la 12 Mkutano wa13 kikao cha kwanza


Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu amesema kuwa utekelezaji wa AMA, upo uwezekano kwa nchi kupata manufaa zaidi ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa mfumo wa udhibiti wa bidhaatiba na hivyo kuweza kudhibiti bidhaa ambazo kwa sasa hazijaanza kudhibitiwa kama vile viambata hai, damu na bidhaa zake, tiba za kijenetiki na chembe msingi

Waziri Mwalimu amesema AMA itasaidia Tanzania kuwezesha kuongeza viwanda vya bidhaa tiba vya hapa nchini na kuwasilisha taarifa kwa nchi wanachama wa AMA za kuomba usajili zenye vigezo vinavyofanana na hivyo kupunguza usumbufu na muda wa kusajili bidhaa zao katika nchi hizo


“AMA itasaidia kuimarika kwa mifumo ya udhibiti wa bidhaa tiba duni na bandia na hivyo kuwezesha kukabiliana na bidhaa tiba zinazopitishwa kwa kutumia njia zisizo rasmi katika mipaka ya nchi jirani”, Mhe. Ummy Mwalimu Waziri wa Afya , leo Bungeni

“Kukua kwa soko la bidhaa tiba za viwanda vya ndani kutokana na kuwianishwa kwa masharti ya usajili wa bidhaa tiba kwa nchi wanachama kama ilivyo ainishwa katika Mkataba wa AMA”, ameeleza Waziri Ummy


Hata hivyo ameongeza kuwa AMA itasaidia usajili na upatikanaji wa bidhaa tiba kwa haraka pamoja na kupunguza gharama zinazotokana na taratibu za usajili wa bidhaa hizo, kwa kuwianisha mifumo ya usajili na kuondoa utaratibu wa sasa ambapo kila nchi huhitaji kukagua viwanda vinavyozalisha bidhaa tiba miongoni mwa nchi wanachama wa AMA


Lakini pia itasaidia uimarishaji mifumo ya udhibiti wa bidhaa tiba duni na bandia miongoni mwa nchi wanachama wa AMA kutokana na kurekebishwa kwa mfumo wa kisheria wa nchi hizo kwa kuzingatia Sheria ya Mfano ya AU iliyopitishwa mwaka 2016


Vile vile amesema AMA itaharakisha upatikanaji wa bidhaa tiba hususan wakati wa dharura na majanga kutokana na kuwa na mifumo ya usajili iliyowianishwa


Aidha amesema pia itarahisisha kupata taarifa kwa urahisi kutoka kwa nchi mbalimbali zilizoridhia na zinazotekeleza Mkataba. Kwa mantiki hiyo, na kwa kutambua umuhimu wa kufikia malengo ya kitaifa na kimataifa kwa ufanisi katika kuimarisha uwezo wa nchi kudhibiti bidhaa tiba na kuhakikisha zinapatikana kwa haraka na zikiwa zenye ubora, ufanisi na salama, Serikali inaiomba Bunge lako lijadili na kuridhia pendekezo hili kwa mujibu wa Ibara ya 63 (3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977