Customer Feedback Centre

Ministry of Health

APOLLO YAANZA TATHMINI UJENZI WA HOSPITALI DAR ES SALAAM

Posted on: November 6th, 2023

Na. WAF - Dar es Salaam


Uongozi wa Kituo cha Umahiri na Ubobezi wa Kimatibabu ‘Apollo Hospitali’ kilichopo nchini India umeanza kutathmini eneo itakapojenga Hospitali jijini Dar es Salaam ambapo uwekezaji huo utakaoleta chachu katika Sekta ya Afya.


Hayo yamesemwa leo Novemba 6, 2023 na Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. John Jingu wakati wa mazungumzo na Rais wa Apollo Group Hospitals, Dkt. K Hari Prasad kilichofanyika Jijini Dar es Salaam. 


Amesema, majadiliano hayo yamefuatia kati ya Rais Samia na uongozi wa Hospitali hiyo yaliyofanyika Oktoba 11 mwaka huu ambapo hadi Sasa ni siku 27 tu zimepita tangu majadiliano hayo yafanyike. 


Aidha, Dkt. Jingu amesema ndani ya miaka mitatu Hospitali hii itakuwa imeshajengwa na inafanya kazi, tuna kila sababu ya kumshukukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona jambo hili ni muhimu ambapo uwekezaji huo utazidi kuboresha huduma za Afya. 


Wakati akiendelea kuelezea umuhimu wa Hospitali hiyo Dkt. Jingu amesema kuwa hatua hiyo ni katika kuhakikisha Tanzania inakua na kituo cha umahiri ukanda wa kusini mwa Africa lakini pia ukanda wa Afrika Mashariki ambapo Tanzania imewekeza katika kuboresha huduma za Afya hivyo kituo hiko cha umahiri kitaongeza utalii wa matibabu na watu wote watakuja kupata huduma za Afya nchini”. Amesema Dkt. Jingu


Kwa upande wake Rais wa Apollo Group Hospitals, Dkt. K Hari Prasad wakati akizungumzia mchakato unaoendelea baada ya kikao cha siku tatu kati ya hospitali hiyo na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Afya amesema wamekuja Tanzania kuanzisha kituo cha matibabu bobezi ili kuongeza ubora wa huduma za Afya nchini. 


“Sisi tunaziba pengo lililopo na hatuji kwa sababu ya mashindano na watoa huduma wengine, tunaamini katika hili na ujio wa bima ya afya kwa wote pia utasaidia watu kupata huduma bora zaidi Tanzania na Baraza la Afrika”. Amesema Dkt. Prasad 


Amesema, katika mazungumzo yao na Rais Dkt. Samia ambapo amesisitiza namna watakavyosaidia kuleta huduma za kibingwa nchini ikiwemo matibabu kwa watoto wenye matatizo ya moyo na hasa yale magonjwa ambayo bado Watanzania wanafuata huduma hizo nchini India.


"Tulisaini makubaliano kati ya Tanzania na India, tumekaa hapa kwa siku tatu, tumeangalia sera zilizopo na kuona eneo ambalo tutawekeza tumefurahi sana na tunaamini miaka miwili ijayo tutaweza kuanzisha huduma kwani tunashauku na hatuna wasiwasi kuwekeza Tanzania”. Amesema Dkt. Prasad


Nae, Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu amesema wamekaa na uongozi wa Apollo kwa siku tatu na kufanya makubaliano kadhaa ikiwemo eneo ambalo Hospitali hiyo itajengwa.