Customer Feedback Centre

Ministry of Health

ALIYEKUWA MGONJWA MOI, ATOA TUZO KWA WAUGUZI

Posted on: August 24th, 2023

Mgonjwa aliyekuwa amelazwa wodi namba 6 “A” katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) ametoa tuzo maalum ya kuwapongeza wahudumu wa wodi hiyo kwa huduma bora wanazotoa kwa wagonjwa.


Mgonjwa Godfrey Mushy alilazwa wodini hapo kwa miezi Mitano kuanzia Oktoba, 15, 2022 kutokana na kupata mivunjiko ya mifupa sehemu mbalimbali za mwili (Polytrauma) na kuruhusiwa Februari 2023 baada ya afya yake kutengamaa.  


Katika tuzo yake hiyo aliyowapatia wauguzi wa MOI, Mushy ameandika  “WAPENDWA WAUGUZI WA WODI NAMBA SITA ‘A” , Nataka kuelezea  kuguswa kwangu na huduma zenu bora mlizonipa katika kipindi chote nilichokaa hapo. Upendo wenu wa hali ya juu kwa kuiona kila hatua ya maisha ni muhimu. 


Nawashukuru kwa huduma zenu! Asanteni kwa kujitoa katika safari hii ya pamoja!


Kwa pamoja tunawapongeza nyie wote! Mikono yenu ya kuponya na mionyo yenu ya kujali ni baraka za kweli kwa mnaowahudumia.


Asanteni kwa juhudi zenu za bila kuchoka na  jitihada zenu za kutoa huduma kwa upendo wa hali ya juu. Kutoka ndani ya mioyo yetu Bwana na Bibi G. Mushy” 


Wauguzi wa wodi hiyo wamemshukuru mteja wao kwa niaba ya MO na kwamba tuzo hiyo imewafariji na kuwaongezea hari ya kutoa huduma bora zaidi katika utekelezaji wa majukumu yao.