MIFUMO YA AFYA KUSOMANA KUANZIA NGAZI YA MSINGI HADI TAIFA – WAZIRI MHAGAMA
Posted on: June 3rd, 2025
Na WAF- Dodoma.
Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama amewahakikishia Wabunge kuwa Serikali inakwenda kuboresha mifumo ya Sekta ya Afya inasomana kuanzia vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi hadi kufikia ngazi ya Taifa ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa haraka pamoja na kuwapunguzia wananchi gharama za matibabu.
Amesema hayo leo Juni 03, 2025 Bungeni Dodoma, wakati akijibu hoja za Wabunge kuhusu matumizi ya TEHAMA katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya.
“Haiwezekani unatoka Songea unakwenda Njombe kwa matibabu unapima, ukienda Mbeya au Dar unapima, kitu ambacho kingeweza kurahisishwa kwa mifumo kusomana,” amesema Waziri Mhagama na kuwahakikishia Wabunge kuwa Serikali itapambana ili kuwa na mifumo ambayo itakuwa ni suluhisho la uhaba wa watumishi pamoja na kupunguza gharama za matibabu.