Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

WARATIBU WA TIBA ASILI WAELEKEZWA KUKEMEA RAMLI CHONGANISHI.

Posted on: May 5th, 2022

Na WAF - MWANZA. 


KAIMU Mkuregenzi Msaidizi anayeshughulikia Tiba Asili na Tiba Mbadala Wizara ya Afya Bi. Lucy Mziray ametoa wito kwa Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala ngazi ya Halmashauri kukemea ramli chonganishi zinazofanywa na baadhi ya Waganga wa tiba asili wasio waaminifu. 


Bi. Lucy ametoa wito huo leo Mei 6 katika ufunguzi wa mafunzo ya Waratibu wa tiba asili wa baadhi ya Halmashauri nchini, mafunzo yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo juu ya shughuli mbalimbali za tiba asili nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza. 


Amesema, wapo baadhi ya Waganga wa tiba asili wanafanya ramli chonganishi jambo ambalo ni kinyume cha taratibu, Sheria na miongozo ya Serikali, hali inayopelekea uminywaji wa haki na uvunjifu wa amani katika ngazi ya familia na jamii kwa ujumla. 


"Nitoe wito kwa Waratibu wote wa tiba asili na tiba mbadala nchini, kuhakikisha wanakemea ramli chonganishi zinazofanywa na baadhi ya Waganga, na hali hii hupelekea kutotenda haki na inaweza kupelekea uvunjifu wa amani katika ngazi zote ikiwemo ngazi ya familia na jamii." Amesema. 


Sambamba na hilo, amesema kuwa, kuanzia mwaka 2018 Kitengo cha Tiba Asili kwa kushirikiana na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala na baadhi ya vyuo vya kitaaluma imefanikiwa kuwapa mafunzo Waganga wa tiba asili 200 kuhusu miiko ,maadili na usafi katika kuandaa dawa za  asili. 


Aidha, ametoa rai kwa Waratibu wa Tiba asili wote waliohudhuria kupeleka ujuzi kwa kuwafundisha na kuwahamasisha waganga wa tiba asili na tiba mbadala juu ya ya sheria, miiko na maadili ya kazi wanazofanya katika jamii na uzingatiaji wa usafi na usalama katika utoaji wa huduma zao, ikiwa pamoja na uandaaji salama wa dawa za asili. 


Kwa upande wake Kaimu Msajili wa Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala Bw. Ndehani Msigwa amewapongeza Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala kwa kuhudhuria mafunzo yenye lengo la kuchochea utoaji wa huduma bora na salama ili kuilinda Afya ya Watanzania. 


Aliendelea kwa kutoa wito kwa Waratibu wa Tiba asili kuhakikisha wanasajili Waganga wote katika maeneo yao na kusajili vituo vyao wanavyotolea huduma ili Watambulike na Wizara pamoja na Baraza linalowasimamia kwa mujibu wa Sheria na taratibu. 


"Bado tunao Wataalamu wengi kwenye maeneo yetu ambao hawajasajiliwa na kwa waliosajiliwa bado vituo vyao havijasajiliwa, hii ni changamoto kubwa ambayo naamini baada ya kutoka kwenye mafunzo haya tutakwenda kuitatua." Amesema Bw. Msigwa. 


Nae, Katibu wa Afya kutoka Balaza la Tiba asili na Tiba mbadala Bw. Patrick Seme amewataka Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala ngazi ya Halmashauri kuratibu matangazo ya tiba asili kwenye vyombo vya habari, na kuchukua hatua kwa wanaotoa na wanaorusha matangazo hayo ambayo hayajapewa kibali na Wizara kupitia Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala kwani matangazo mengi hupotosha umma juu ya uwezo wa kutibu. 


"Mkakemee vitendo vibaya vinavyofanywa na baadhi ya Waganga wa Tiba Asili  ambavyo vinakiuka sheria ya Tiba Asili ya 2002 ikiwa ni pamoja na utoaji wa matangazo ya huduma za tiba asili ambayo hayajapekuliwa na kupewa kibali na Baraza la Tiba Asili na utoaji wa huduma za tiba asili bila kusajiliwa." Amesema. 


Mwisho.