Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

WAGONJWA 210,382 WAPATIWA HUDUMA ZA UTENGAMAO

Posted on: May 18th, 2024

UTEKELEZAJI WA BAJETI YA WIZARA YA AFYA 2023/24

Na WAF - Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuratibu utoaji wa huduma za utengamao kwa wagonjwa 210,382 nchini hususan kwa watu wenye ulemavu na wenye mahitaji maalum ikiwemo watoto na wazee kwa kipindi cha Julai 2023 hadi Machi 2024.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema hayo Bungeni Mei 13, 2024 akiwa anawasilisha hotuba yake ya bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2024/25 akielezea utekelezaji wa majukumu ya Wizara katika utoaji wa huduma za Kinga nchini.

"Katika kipindi hicho huduma zilitolewa ni pamoja na Fiziotherapia wateja 177,417, tiba kazi (Occupational Therapy) wateja 25,245, Matamshi na Lugha (Speech and Language Therapy) wateja 1,674, Vifaa Tiba Saidizi (Assistive Devices) wateja 4,234." Amesema Waziri Ummy

Aidha, Waziri Ummy amesema viungo tiba na viungo tiba saidizi (Prosthesis and Orthosis) vilitengenezwa na kugawiwa kwa wateja 1,812 ili kuimarisha huduma za Utengamao katika Hospitali Saba ambazo zimeweza kutoa seti Tatu kati ya Nne ya huduma za utengamao.

"Huduma hizo ni pamoja na Fiziotherapia, 'Occupational Therapy', Prosthesis pamoja na Orthosis." Amesema Waziri Ummy

Wakati Waziri @ummymwalimu akiendelea kusoma bajeti ya Wizara ya Afya Bungeni amesema Wizara inaendelea kujenga uwezo kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa zilizobaki ili kuhakikisha upatikanaji wa wataalam wa huduma za Utengamao wanapatikana.

"Ili kufikia lengo hilo kozi mpya Mbili katika ngazi ya Shahada zimeanzishwa katika Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) ambazo ni Speech and language therapy yenye wadahiliwa 15 na occupational therapy yenye wadahiliwa 30 na kufanya jumla ya wadahiliwa kuwa 45 wanaoendelea na mafunzo hayo." Amesema Waziir Ummy