Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

WANANCHI ZAIDI YA 12,000 WANUFAIKA NA KAMBI YA MADAKTARI BINGWA WA RAIS SAMIA

Posted on: May 12th, 2025

Na WAF, Tanga


Mkuu wa mkoa wa Tanga Mhe. Dkt. Batilda Salha Burian amesema zaidi ya wananchi 12,000 wamenufaika kwa kupatiwa huduma za kibingwa na madaktari bingwa wa Rais Samia kwa awamu tatu zilizopita.


Mhe. Dkt. Burian ameyasema hayo Mei 12, 2025 wakati akipokea na kufungua kambi ya siku sita ya Madaktari Bingwa wa Rais Samia mkoa wa Tanga kwa awamu ya nne.


Amesema kambi hizo zimesaidia sana kupunguza rufaa kwa wagonjwa, gharama kwa familia na usumbufu wa kufuata huduma hizo za kibingwa mbali na maenei yao


“Wengine walipatiwa huduma za upasuaji hapa hapa katika hospitali zao za halmashauri , tunawashukuru sana kwa kujitoa kwenu na kazi kubwa mliyoifanya ya kuwapatia huduma wananchi wa mkoa wa Tanga,” amesema Mhe. Dkt. Buriani.


Aidha, ameeleza kuwa ujio wa madaktari bingwa hao ni muendelezo wa kutekeleza wa dhamira ya dhati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kufikiwa kwa urahisi karibu na maeneo yao.


“Sisi kama mkoa tumeshuhudia mafanikio makubwa kwenye sekta ya Afya ya kuongezewa vituo vya kutolea huduma za afya 446 kutoka 325 ni sawa na ongezeko vituo 121, zahanati 389 kutoka 287, vituo vya Afya 46 kutoka 31 na hospitali 11 kutoka saba (7) na mkoa una watumishi wa afya 3,887 waliogawanywa katika vituo mbalimbali na haya yote yametokea katika kipindi cha miaka nne ya Rais Dkt. Samia,” amefafanua Dkt.Burian.


Akitoa salamu za Wizara ya Afya, Afisa Progamu kutoka Idara ya Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto Bw. Michael Mbele amesema kupelekwa kwa madaktari bingwa hao kwenye hospitali zao za halmashauri kunawasaidia kupata matibabu ya kibingwa ambayo walikuwa wanashindwa kuyapata kwa sababu za kiuchumi, muda na umbali.


“Kwa awamu hii pia tumeongeza daktari bingwa wa magonjwa ya pua, koo na masikio  na wataalam wa ukunga wabobezi, tunatarajia pia kutoa mafunzo kwa timu zilizopo katika hospitali,” amesema Bw. Mbele.


Naye Daktari Bingwa wa Kinywa na Meno Dkt. John Sijaona amesema wamejipanga vizuri kutoa huduma kwa wananchi na kumpongeza Rais Dkt. Samia kwa kupeleka vifaa vya kisasa vya kinywa na meno katika hospitali za wilaya ambavyo vitarahisisha utoaji wa huduma za kinywa na meno wakati wa kambi hizo.