Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

UPIMAJI WA AFYA UNAENDELEA MKOANI KIGOMA

Posted on: May 27th, 2022

Na. WAF - Kigoma 


Maadhimisho ya Hedhi Salama Duniani yametoa fursa ya upimaji afya wa Magonjwa mbalimbali pamoja na utoaji wa elimu juu ya Afya unaendele katika viwanja vya Mwanga Community Center uliopo mkoani Kigoma. 


Maadhimisho hayo yameanza rasmi Mei 24, 2022 katika viwanja hivyo yanaenda sambamba na utoaji wa huduma za upimaji wa Magonjwa na utoaji wa elimu na kutarajiwa kumalizika kwa kilele Mei 28, 2022.


Maadhimisho hayo ya kilele yatahudhuriwa na wananchi pamoja viongozi mbalimbali wa Wizara ya Afya ambapo mgeni rasmi atakuwa Mke wa Makamu wa Rais wa Tanzania Mama Mbonimpae Mpango.


Miongoni mwa huduma za upimaji wa magonjwa zinazotolewa hapo ni pamoja na upimaji wa Saratani ya mlango wa kizazi, UVIKO-19,UKIMWI, shinikizo la damu (Presha), upimaji wa Sukari pamoja na uzito na huduma hizo zote zinatolewa bure.


Aidha, elimu pia inatolewa juu ya Uzazi wa mpango, namna nzuri ya ulaji wa vyakula (lishe)na ukweli kuhusu Covid-19.


Hivyo, wakazi wote na wananchi  wa Mkoa Kigoma wanakaribishwa kujitokeza kwa wingi kwenda kupata huduma zote za upimaji pamoja na elimu zinazotolewa katika viwanja hivyo Bure.


Hata hivyo Maadhimisho hayo siku ya kilele May 28, 2022 yatasindikizwa na mbio za  km 5, zitakazo anzia katika viwanja vya Mwanga community center kuanzia saa 1:00 asubuhi zikiongozwa na viongozi kutoka wizara ya Afya, wanafunzi pamoja na wananchi. 


Maadhimisho hayo ya Hedhi Salama Duniani, kitaifa yanafanyika Mkoani Kigoma katika viwanja vya Mwanga Community Center yenye kauli mbiu isemayo "HEDHI NI TUNU NA MSINGI WA AFYA, DHAMIRIA KUWEKEZA KATIKA NYANJA ZOTE."\


MWISHO