Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

TUNDUMA YAPONGEZWA KWA KUAJIRI WATUMISHI WA AFYA WA MKATABA

Posted on: September 12th, 2023

Na. WAF - Songwe


Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amewapongeza viongozi wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma kwa kuajiri watumishi wa Afya wa mkataba kwa kutumia mapato ya ndani.


Waziri Ummy ameyasema hayo Septemba 12, 2023 alipokuwa akizungumza na watumishi katika kituo cha Afya Mji wa Tunduma wakati akiendeleza ziara yake ya siku Tatu katika Mkoa huo wa Songwe. 


“Kipekee nimpongeze sana Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma pamoja na Mkurugenzi Mtendaji kwa kutumia mapato ya ndani kuajiri watumishi wa Afya wa Mkataba”. Amesema Waziri Ummy 


Aidha, Waziri Ummy ametaka Halmashauri nyingine ziige mfano huo mzuri wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma kwa sababu fedha za mapato ya ndani zinakusanywa kutoka kwa wananchi hivyo ni bora kutumia fedha hizo kutatua kero za wananchi. 


Pia, Waziri Ummy amesema upatikanaji wa dawa katika Halmashauri ya Mji wa Tunduma upo vizuri ambapo dawa zinapatikana kwa asilimia 94.


“Asilimia 94 kubwa na nzuri lakini hizo asilimia Sita iliyobaki pia hatutaki kusikia dawa hakuna hasa katika awamu hii ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwakuwa anatoa fedha za dawa kwa 100% kwa kila Mwaka”. Amesema Waziri Ummy


Hata hivyo, Waziri Ummy ametoa maelekezo kwa Mganga Mkuu wa Mkoa pamoja na timu yake kuhakikisha wanafanya kaguzi za mara kwa mara za kuangalia upatikanaji wa dawa katika Mkoa huo. 


“Hatutaki kusikia mtu anakosa dawa wakati fedha za dawa zipo, lakini kwa ujumla dawa zote muhimu zipo na hii ni kutokana na juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuwajiali Watanzania”. Amesema Waziri Ummy