Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

TANZANIA BADO YAKABILIWA NA UHABA WA DAMU SALAMA

Posted on: June 14th, 2022

Tanzania haijafikia lengo la ukusanyaji wa damu salama kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani linalopendekeza nchi kukusanywa idadi ya chupa za damu ambazo ni sawa na asilimia 1 ya idadi ya wananchi waliopo kwenye nchi au eneo hilo kwa wakati huo.

Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Omary Mgumba kwa niaba ya Waziri wa afya Mhe. Ummy Mwalimu wakati alipokua mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya siku ya mchangia damu duniani ambayo kitaifa yamefanyika katika mji wa Tunduma mkoani Songwe.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Omary Mgumba.

Mgumba amesema nchi ya Tanzania, inakadiriwa kuwa na wananchi milioni 55, inatakiwa kukusanya chupa za damu 550,000 ambayo ni sawa na asilimia 100 ya mahitaji ya nchi ikilinganishwa na idadi ya wananchi waliopo.
“Takwimu za ukusanyaji damu, zimeonyesha kuwa na mafanikio ya kuongozeka kwa ukusanyaji damu mwaka hadi mwaka. Mwaka 2017/2018 jumla ya chupa za damu 257,557 ambayo ni sawa na 45% ya mahitaji zilikusanywa, kufanyiwa vipimo vya maabara, na kusambazwa. Idadi hii imeongezeka hadi kufikia chupa 312,714 sawa na 57% ya mahitaji kwa mwaka 2019/2020, na kufikia 331,279 ambayo ni sawa na 60% ya mahitaji ya nchi kwa mwaka 2020/2021 lakini bado ukusanyaji huu haijakidhi mahitaji”. Amesema Mgumba.

Mkuu wa Mkoa huyo amesema pamoja na ongezezo hilo, bado nchi haijafikia malengo ya kukusanya chupa 550,000 ingawa chupa zilizokusanya mwaka 2022/2021 ni chupa 331,279 sawa na asilimia sitini (60%), bado kuna pungufu ya chupa 218,721 sawa na 40% ya mahitaji ya nchi.

Mhe. Mgumba amesema bado kuna kazi ya kufanya ya kuhakikisha hilo pengo la asilimia 40 linazibwa ili kukidhi mahitaji ya damu na kuhakikisha kuwa wale wote ambao wanahitaji kuongezewa damu wanapata huduma hio kwa wakati, na kwa viwango na kiasi kinachohitajika.

Aidha, ameomba ushiriki wa taasisi na vikundi mbalimbali katika kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuchangia damu ili kuweza kupunguza na hatimae kuondoa pengo lililobaki na kuondoa kabisa uhaba wa damu nchini.
Maadhimisho ya siku ya mchangia damu duniani mwaka huu yamebebwa na kaulimbiu inayosema kuchangia damu ni kitendo cha mshikamano tuungane kuokoa Maisha.