Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

SERIKALI YATUMIA BILIONI 346.4 KUTIBU WAGONJWA WA KISUKARI NA TEZI DUME

Posted on: February 6th, 2024

Na WAF - Dodoma


Serikali imesema kuwa gharama ya kutibu wagonjwa wa Sukari kwa mwaka ni shilingi bilioni 300, na gharama za kutibu wagonjwa wote wa tezi dume ni shilingi bilioni 46.42 hivyo kupelekea jumla ya gharama za matibabu kwa magonjwa haya mawili kufikia shilingi bilioni 346.42.


Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel leo Bungeni Jijini Dodoma wakati akijibu swali namba 98 kwa niaba ya Waziri wa Afya, Mhe. Ummy Mwalimu ambapo swali hilo limeulizwa na Mbunge wa Igalula, Mhe. Venant Daud aliyeuliza Je, Serikali haioni haja ya kutoa msamaha wa matibabu kwa wagonjwa wa sukari na tezi dume nchini.


Dkt. Mollel ameeleza kuwa gharama za matibabu ya magonjwa hayo mawili ni kubwa sana wakati bajeti ya dawa lna vifaa tiba kwa mwaka ni shilingi bilioni 200. 


“Ikitokea huduma ya matibabu kwa magonjwa haya mawili kutolewa bure kutasababisha huduma nyingine katika nchi kusimama”. Amesema Dkt. Mollel. 


Aidha, amesema Serikali inasisitiza utekelezaji wa Sera ya Afya ya Mwaka 2007, ya kutoa huduma ya Msamaha kwa wananchi wasio na uwezo wa kulipia huduma za afya hata hivyo, wenye uwezo wa kulipia wataendelea kuchangia.


Dkt. Mollel ameongeza kuwa mwaka 2022/2023 gharama ya msamaha wa matibabu kwa wagonjwa wa sukari na saratani ya tezi dume ilikuwa kiasi cha shilingi bilioni 70.4


Vile vile Dkt. Mollel amesisitiza viongozi wa Mamlaka za mikoa na Serikali za mitaa kusimamia sekta ya afya kikamilifu ili kuleta ubora wa huduma ili kutekelza azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kila Mtanzania kupata huduma bora za afya.