Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

RAIS SAMIA AZINDUA HOSPITALI YA KANDA KUSINI, ASISITIZA UTOAJI WA HUDUMA BORA ZA AFYA KWA WANANCHI NA KWA LUGHA NZURI.

Posted on: September 15th, 2023


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan mapema leo hii Septemba 15, 2023 amezindua Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini iliyopo Mtwara.


Rais Samia amesema kuwa kukamilika kwa Hospitali hiyo ambayo ina watalaam, vifaa na vifaatiba vya kisasa itasaidia watu wa Kanda ya Kusini inayojumuisha Mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma kupata uhakika wa huduma za matibabu ya kibingwa karibu na maeneo yao.


“Wagonjwa wote wenye matatizo makubwa watakuja hapa, jengo hili litumike kutoa huduma za afya” amesema Rais Samia.


Rais Samia amesema kuwa kazi ya watumishi wa afya ni kuokoa maisha ya watu hivyo watumishi hao wajitumie kufanya kazi kwa kuwa Serikali imewekeza kwenye miundombinu, vifaa na dawa na wao watimize wajibu wao 


Tunahitaji matunzo ya jengo hili, vifaa na huduma kwa wananchi kwa lugha nzuri, kila mtu amepangiwa jukumu lake na Mwenyezi Mungu, tumridhishe Mungu kwa huduma tunazozitoa, nawatakia kila la kheri” amesema Rais Samia huku akiongezea kuwa changamoto zilizopo za watumishi zitaendelea kufanyiwa kazi kwa haraka.