Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

MADAKTARI BINGWA WA MAMA SAMIA WAJENGA UWEZO KWA WATUMISHI WA AFYA MOROGORO

Posted on: March 22nd, 2024



Na WAF, Morogoro

Madaktari bingwa wa Mama Samia wamefanya kazi ya kujenga uwezo kwa watumishi wa afya katika vituo vya Ngerengere na Chazi, mkoani Morogoro ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Hayo yamebainishwa na Dkt. Mariam Gaitan, Machi 22,2024 wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi waliopo ngazi ya msingi ili kuboresha huduma za mama na mtoto kupitia huduma za mkoba.

Dkt. Gaitan amesema zaidi ya wananchi 40 wamepatiwa huduma za kibingwa, hatua ambayo imepunguza rufaa za wagonjwa na kusaidia kuboresha afya ya jamii.

"Zoezi la Mama la Tuwavushe Salama, tumefanikiwa kuwafikia wagonjwa waliokuwa na hitaji la huduma za madaktari bingwa, kwanai tumetoa huduma kwa zaidi ya watu 40 na kutatua changamoto zilizokuwa zinawakabili" amesema Dkt. Mariam.

Akizungumza wakati wa Semina hiyo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Kusirye Ukio, amesema kuwa, uwepo wa jopo la madaktari hao katika mkoa huo ni jitihada za kupunguza vifo vya mama na mtoto ikiwa ni sehemu ya juhudi za Dkt. Rais Samia katika kuboresha kwenye sekta ya afya.

Kwa upande wake Daktari kutoka Kituo cha Afya Ngerengere, Clement Nkinga, hakusita kuonesha furaha yake kuhusu ujuzi waliopatiwa na madaktari bingwa hao, akibainisha kuwa utawasaidia kupunguza idadi ya rufaa za wagonjwa kwakua wana uwezo wa kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi.

Moja ya mkazi wa Kiburugwa mkoani Morogoro, Rehema Jackson, amemshukuru Rais Samia kwa kuleta madaktari bingwa katika vituo vya afya na kutoa ombi kwa madaktari hao kuendelea kufika mara kwa mara katika vituo hivyo ili kutoa huduma na kuendelea kuboresha afya ndani ya jamii.