Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

MABINTI ZAIDI YA MILIONI TANO KUPATIWA CHANJO YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI 2024.

Posted on: April 12th, 2024


Na. WAF – Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya imepanga kuendelea utoaji wa chanjo kwa watoto zaidi ya milioni tano ya ugonjwa wa Saratani ya mlango wa kizazi (HPV) kwa mabinti wa miaka tisa hadi kumi na nne ili kuwakinga na vimelea vya ugojwa huo.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi wa kitengo cha elimu ya Afya kwa umma Dkt. Tumaini Haonga leo tarehe 13 Aprili, 2024 wakati wa semina ya waandishi wa habari kuhusu chanjo ya Saratani ya mlango wa kizazi jijini Dodoma.


Amesema, chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi itatolewa kwa mabinti zaidi ya milioni tano wenye umri wa kuanzia miaka tisa hadi kumi na minne kwa dozi moja ambapo awali ilikuwa ikitolewa kwa watoto wenye umri wa miaka kumi na minne tu kwa dozi mbili.

“Kufuatia tafiti ya WHO na kwa kuzingatia mingozo ya wizara yetu ya afya imeona chanjo ya HPV inaweza kuwa na ufanisi wa kutosha kwa kumkinga mtoto kutokana na vimelea vya saratani ya mlango wa kizazi hata kwa dozi moja, ambapo awali tulikuwa tunawapatia dozi mara mbili, nitoe rai kwa watanzania kuwatoa watoto hao ili kuweza kupatiwa chanjo hii”. Amesema Dkt. Haonga.

Aidha, Dkt. Haonga amevitaka vyombo vya habari kote nchini kutumia  taaluma zao kuhamasisha na kuelimisha na kuwapa ufafanuzi wananchi juu ya masuala mazima ya afya hususani kuhusu ugonjwa wa saratani na mlango wa kizazi na chanjo yake kwa sababu wananchi wengi wanategemea kupata taarifa kupitia vyombvo vya habari.

 “Nitoa wito kwa wanahabari kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhakikisha taarifa, elimu na uhamasishwaji wa jamii kuhusu chanjo hii zinawafikia watanzania, ninyi wanahabari mna vyanzo vingi vinavyoweza kuwafikia watanzania kwa wingi hivyo mkatoe  taarifa kuhusu afya ili kufikia dhima ya Serikali ya kuwakinga wananchi na saratani ya mlango wa kizazi na kuhakikisha tunakuwa na taifa lenye afya bora”. Amesisitiza Dkt. Haonga.

Pia amewasisitiza watanzania wote kuwa na desturi ya kupima afya zao mara kwa mara ili kuwahi kuchukua hatua stahiki pindi wanapobainika wana changamoto ya ugonjwa.

Awali akitoa wasilisho  Afisa Progamu wa Mpango wa Taifa wa Chanjo Bi. Lotalis Gadau amesema lengo la kampeni ya chanjo ya saratani ya kizazi ni kuwapa kinga mabinti wa miaka tisa hadi kumi na nne na kuzuia kuenea kwa maambukizi ya saratani ya mlango wa kizazi kwa wanawake hapo baadae.

“Tunalenga kuwapatia mabinti wenye umri wa miaka tisa hadi kumi na nne kwa sababu wanakuwa hawajaanza kujamiana ili kumkinga na virusi vya saratani ya mlango wa kizazi kwa sababu virusi hivyo vinaambukizwa kwa njia ya kujamiana na mmoja ya athari ya ungonjwa huu usipogundulika mapema ni kifo”. Amesema Bi. Gadau.

Mwisho, amesema inakadiriwa kwamba takribani wanawake zaidi ya elfu kumi wanapata saratani ya mlango wa kizazi kila mwaka na wanawake zaidi ya elf sita hupoteza maisha pia amewahasa wanawake na mabinti kufanya vipimo vya saratani ya mlango wa kizazi ili kujua afya zao mapema.