Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

KAMBI YA MADAKTARI BINGWA, BINGWA BOBEZI IMESTAWISHA UTENDAJI WA KAZI GEITA

Posted on: April 30th, 2024



Na WAF - GEITA

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya ndani wa Hospitali ya Rufaa Geita Dkt. Sabrina Kumlin amesema Kambi ya Madaktari Bingwa na Bingwa Bobezi imestawisha utendaji wa kazi kwa kuongeza tija na ufanisi katika utendaji wao.

Dkt. Sablina pamoja na wataalamu wengine wakizungumza kwa Nyakati tofauti wamesema, Kambi ya Madaktari Bingwa iliyoanza Aprili 29, 2024 imewawezesha madaktari kubadilishana uzoefu pamoja na kutatua changamoto za wagonjwa kwa wakati.

"Jopo hili la Madaktari, uzofu wetu unatofautiana, yawezekana mimi nikakutana na jambo kwa mara ya kwanza, lakini tatizo hilo hilo mwenzangu alisha kutana nalo kabla, hivyo tunashauriana kwa haraka na kupata ufumbuzi.” Amesema Dkt. Sabrina

Kwa upande wake Daktari Mbobezi wa wanawake na uzazi Dkt. Ndulila Samweli wa Hoapitali ya Sekouture Mwanza, amesema, hatua yakuwafikia wananchi kwenye maeneo yao imewawezesha wengi kujitokeza.

"Huduma hizi za mkoba tungezishusha hadi ngazi ya Wilaya kwa kuwa uzoefu unaonesha wanachi wengi hushindwa kutoka kwenda mbali kupata matibabu na kumfanya mgonjwa kuendelea kujenga usugu wa ugonjwa, lakini tunapowafuata wengi wanajitokeza.” Amesema Dkt. Ndulila.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Mifupa Dkt. Zablon Saguta amesema ndani ya siku Moja wamekutana na wananchi wenye shida ya mifupa wapatao 70 kwa haraka, sio rahisi watu wote hawa kuhudumiwa na mtu mmoja.

"Idadi hii itaweza kuongezeka kutokana na wanachi kupeana taarifa hivyo unaweza kujiuliza watu wote hao walikuwa na matatizo ya mifupa lakini wameibuliwa na kambi hii ya huduma ya Mkoba.” Amesema Dkt. Saguta

Katika hatua nyingine, Mwalimu mstaafu Bibi Ester Kizuguto ambae ni mkaazi wa Kata ya Mkolani Wilaya ya Geita na mkoani Geita, ameishuru Serikali kwa hatua yake yakusogeza huduma za mkoba za Madaktari Bingwa na Bobezi kwani zimewarahisishia huduma.

Jumla ya Madaktari Bingwa, Bingwa Bobezi 32 wapo Mkoani hapo kuanzja Aprili 29 hadi Mei 3, 2024 kwa ajili ya kuhudumia wananchi kwa kaulimbiu isemeyo “Madaktari wa Dkt. Samia Kanda ya Ziwa Tumekufikia, Karibu Tukuhudumie.”

MWISHO