Wizara Ya Afya

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YATOA USHAURI KWA SERIKALI

Posted on: May 11th, 2026

Na. Aisha Swahibu, WAF - Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI imeitaka Serikali kuendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha sekta ya afya nchini kwa kushughulikia changamoto mbalimbali zinazokwamisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Ushauri huo umetolewa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa na kimataifa ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango Mkakati wa Sekta ya Afya pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya 2030.

Haya yamesemwa na Makamu Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya Ukimwi Dkt. Zeyana Abdallah Hamid Kwa niaba ya Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya Ukimwi Dkt. Johanes Lukumai akiwasilisha maoni ya kamati hiyo kuhusu makadirio na matumizi ya bajeti ya wizara ya afya mwaka wa fedha 2026/27, leo Mei 11, 2026, bungeni jijini Dodoma.

Amesema kuwa Kamati inaishauri Serikali kuendelea kutoa vibali vya ajira kwa kada zenye upungufu mkubwa pamoja na kuongeza ufadhili wa masomo kwa wataalamu wa afya wakiwemo madaktari bingwa na bobezi.

Aidha, Dkt. Zeyana ameitaka Serikali kuhakikisha vibali vya ajira vinazingatia mahitaji halisi ya taasisi husika na kuwapa kipaumbele wataalamu wanaojitolea katika hospitali mbalimbali nchini ili kuongeza nguvu kazi kwenye sekta hiyo muhimu.

Pia, Dkt. Zeyana ameeleza kuwa Kamati imeishauri Serikali kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli kwa kuzijengea uwezo taasisi zake katika mifumo ya ukusanyaji mapato na utoaji wa huduma bora, hatua itakayosaidia kuongeza uwajibikaji kwa viongozi na watumishi wa sekta hiyo.

Kuhusu miradi ya Hospitali za Rufaa za Mikoa, Kamati imeitaka Serikali kutoa kipaumbele kwa miradi iliyoanza muda mrefu ili ikamilike mapema. Aidha, ujenzi wa miundombinu hiyo unatakiwa kwenda sambamba na upatikanaji wa vifaa tiba ili kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Zeyana amesema kuwa Kamati pia imeitaka Serikali kutoa mtaji wa Shilingi bilioni 300 kwa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) pamoja na kulipa deni la zaidi ya Shilingi bilioni 302 linalodaiwa na taasisi hiyo, hatua itakayosaidia kuimarisha upatikanaji wa dawa na bidhaa nyingin