KAMATI YA BUNGE YAKOSHWA UWEKEZAJI SEKTA YA AFYA
Posted on: March 15th, 2025
Na WAF-Simiyu
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, Mhe. Hassan Mtenga, amepongeza juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya, akisema mafanikio haya yanapaswa kusimuliwa kwa Watanzania wote.
Akizungumza wakati wa ziara ya kamati yake katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu, Mhe. Mtenga amesema kuwa Serikali imefanikiwa kupunguza rufaa zaidi ya 5,000 kutoka mikoa ya Mara na Simiyu, hatua iliyopunguza gharama za matibabu na usafiri kwa wananchi.
“Serikali imewekeza zaidi ya Shilingi Bilioni 2.7 kununua vifaa tiba vya kisasa kama CT scan, Digital X-ray, na ventilators. Hii imesaidia kupunguza rufaa za nje ya mkoa na kuboresha huduma za kibingwa,” amesema Mhe. Mtenga.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, amesema kuwa kutokana na uwekezaji huu mkubwa, Rais Samia amependekezwa kuwa mgombea pekee wa urais, kama ishara ya kutambua juhudi zake za dhati katika kuboresha huduma za afya na kuhakikisha kila Mtanzania anapata matibabu bora karibu na nyumbani.
Aidha, Dkt. Mollel amesema chini ya uongozi wa Dkt. Samia, Serikali imefanikisha ujenzi wa jengo jipya la huduma za mama na mtoto lenye vitanda 140, ambalo limepunguza msongamano na kuboresha huduma za dharura za uzazi. Vilevile, mtambo mpya wa kuzalisha hewa tiba wenye thamani ya zaidi ya Shilingi Milioni 650 umeanzishwa, ukihakikisha wagonjwa mahututi wanapata huduma kwa wakati.
Pia amebainisha kuwa katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Dkt. Samia, hospitali imeongeza idadi ya madaktari bingwa, wauguzi, na watumishi wengine wa afya, huku Serikali ikiendelea kugharamia mafunzo ya kibingwa kwa madaktari wa ndani na nje ya nchi.
Mafanikio haya ni kielelezo cha uongozi thabiti na dhamira ya kweli ya Dkt. Samia ya kuboresha ustawi wa wananchi, kwani sababu hizi zimeipa CCM imani ya kumteua kuwa mgombea pekee wa urais kwenye uchaguzi ujao.