Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

HAKUNA KILICHOSIMAMA KATIKA MIRADI YA AFYA - MHE. NYONGO

Posted on: March 16th, 2024


Na. WAF - Chato, Geita

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mhe. Stanslaus Nyongo ameipongeza Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuendeleza miradi ya Afya ambapo hadi sasa hakuna mradi uliokwama.

Mhe. Nyongo amesema hayo leo Machi 16, 2024 baada ya kutembelea miradi ya ujenzi wa jengo la wodi la ghorofa Mbili lenye uwezo wa vitanda 201 pamoja na jengo la Mionzi yanayojengwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Chato akiambatana na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu pamoja na wajumbe wa Kamati hiyo.

Amesema, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuja na slogan ya kusema ‘Hakuna Kilichosimama’ hivyo kama Kamati wamethibitisha hilo baada ya kutembelea katika Haspitali ya Kanda ya Chato na kuona kasi ya ujenzi wa majengo hayo yanavyokwenda vizuri bila kikwazo chochote.

“Sisi kama Kamati tumeridhika baada ya kuona ujenzi unavyoendelea, tumeongea na wakandarasi wanapata fedha kwa wakati kwa hiyo tunampongeza sana Mhe. Rais Samia pamoja na Waziri wa Afya kwa kusimamia maendeleo haya.” Amesema Mhe. Nyongo

Aidha, Mhe. Nyongo ameitaka Wizara ya Afya kuendelea kuwekeza katika ukanda huo wa ziwa ili kupunguza msongamano katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), wagonjwa wa Moyo wanaotokea Kanda ya ziwa waweze kutibiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Chato.

“Tunaona watu wa Kanda ya Ziwa wengi wanamatatizo ya Moyo, kwa hiyo ni vizuri kituo hiki kikamalizika kwa wakati ili wananchi wapate huduma hapa ambapo pia tutaendelea kumuenzi Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kwa uwekezaji tunamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anamuenzikwa vitendo.” Amesema Mhe. Nyongo