Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

DOLA MILIONI 250 KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA YA UZAZI MAMA NA MTOTO.

Posted on: November 7th, 2023

Na. WAF - Dodoma


Katika kuendeleza juhudi za uboreshaji huduma za Afya ya Uzazi Mama na Mtoto, Serikali kupitia Wizara ya Afya inatekeleza programu ya uboreshaji huduma hizo ujulikanao kwa jina la ‘Tanzania Martenal and Child Health Investment Program (TMCHIP)’ kwa miaka Mitano ukiwa na thamani ya zaidi ya Dola Milioni 250.


Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu alipokutana na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Dunia Dkt. Juan Pablo Urine kwenye kikao kilicholenga kujadili uboreshaji wa huduma za Afya nchini.


“Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Benki ya Dunia inatekeleza program hii ya miaka Mitano kuanzia Januari 2023 hadi Disemba 2027, Programu hii inalenga kuboresha ubora wa huduma za Afya ya uzazi, mama na mtoto nchini”. Amesema Waziri Ummy


Waziri Ummy amesema kuwa kupitia programu hiyo, Serikali itaboresha vyumba/vituo 15 vya uangalizi wa Watoto njiti (NICU) katika Hospitali za Rufaa za Mikoa, kuboresha NICU 10 katika vyuo vya Afya na kuboresha Vituo vya ukusanyaji wa Damu Salam Sita.


“Tunatarajia kutoa mafunzo ya kitaalam kwa watoa huduma zaidi ya 10,000 pamoja na kutoa mafunzo elekezi kazini kwa wataalam zaidi ya 8,000 nchi nzima ili waweze kutoa huduma bora za afya ya uzazi mama na mtoto”. Amesema Waziri Ummy 


Waziri Ummy amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea na mageuzi makubwa ya utoaji wa huduma za afya nchini kulingana na Mpango Mkakati wa tano wa Sekta ya Afya na Mpango wa Maendeleo wa Miaka mitano wa Tanzania.


Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa jitihada zinahitajika zaidi na ushiriki wa wadau katika kuboresha zaidi huduma za Afya nchini na kuomba ushirikiano wa Benki ya Dunia katika eneo la uimarishaji wa huduma kutoka kwa watoa huduma za Afya ngazi ya jamii, ugharamiaji wa Bima ya Afya kwa Wote pamoja na kuweka mifumo imara ya huduma za dharura na udhibiti wa majanga.


Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Dunia Dkt. Juan Pablo Uribe ameipongeza Tanzania kupitia Wizara ya Afya kwa kuwa na mfumo wa kupeleka wagonjwa haraka kwa kutumia magari ya dharura (M-Mama).


“Lakini pia niwapongeze kwa kujali Afya za Watanzania kwenye upande wa Vijana na Lishe”. Amesema Dkt. Uribe


Mwisho, ameishauri Serikali kuwa na mfumo kama wa M-Mama kwa kutumia ‘Ambulance’ ili kisaidia zaidi wananchi hasa kina mama pindi wanapohitaji huduma za dharura ili kuweza kuwasaidia kwa haraka.