Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

DKT. JINGU AKOSHWA NA HUDUMA ZINAZOTOLEWA HOSPITALI YA MKOA MOROGORO

Posted on: November 14th, 2023



Na. WAF - Morogoro

Huduma zinazotolewa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro zinaenda sambamba na malengo ya Sekta ya Afya kwa kutoa huduma zinazozingatia mipango ya uboreshaji wa huduma za Afya nchini.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. John Jingu amesema hayo leo Novemba 14, 2023 wakati akizungumza na watumishi na watoa huduma za Afya katika Hospitali hiyo.

Dkt. Jingu ametembelea wodi mbalimbali ikiwemo wodi ya uangalizi maalum ya watoto, wodi ya wanaume ya upasuaji wa mifupa, wodi ya watoto pamoja na wodi ya watoto njiti ambapo amezungumza na wagonjwa wakimueleza huduma nzuri wanazopata katika Hospitali hiyo.

“Kwakweli nimezunguka wodi mbalimbali katika Hospitali hii ikiwemo wodi ya watoto njiti na nimeona huduma nzuri na wenyewe wamesifia lakini pia nimeona watoa huduma wakifanya kazi zao vizuri, nawapongeza sana kwa hili.” Amesema Dkt. Jingu

Aidha, Dkt. Jingu pamoja na kutoa pongezi kwa watumishi hao amewataka kuendelea kutoa huduma kwa kuzingatia taaluma zao, maadili ya kazi pamoja na weledi katika kuwahudumia wagonjwa.

“Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaimani na ninyi hivyo kuendelea Imani hiyo kwa Mhe. Rais mnatakiwa kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, weledi na taaluma mliyokuwa nayo ili kuleta ahueni na nafuu kwa wanaoteswa na Magonjwa mbalimbali.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu amewashukuru na kuwapongezi watoa huduma wote wa Hospitali kwa kutambua kazi kubwa wanayoifanya kwakuwa kazi hiyo ni yenye thawabu nyingi.

“Tunatambua kuwa kazi ya kumhudumia mgonjwa unaweza kupata sifa nzuri au lawama au laana hivyo ni vyema kuzingatia majukumu yetu wakati wa kazi kwa kufuata taratibu na miongozo ya taaluma zetu.” Amesema Prof. Nagu