BILIONI 17.8 ZATUMIKA KUNUNUA MITAMBO YA UCHUNGUZI WA KIMAABARA.
Posted on: March 15th, 2025
Na. WAF, Dodoma
Serikali kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imewekeza mitambo na vifaa vya kisasa vya uchunguzi vyenye thamani ya Shilingi Bilioni 17.8 ikiwemo mitambo mikubwa 16 na midogo 274 kwa ajili ya kuboresha huduma za uchunguzi wa kisayansi wa kimaabara ndani ya kipindi cha miaka minne.
Hayo yameelezwa Machi 14, 2025 na Mkemia Mkuu wa Serikali Dkt. Fidelice Mafumiko wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, kuhusu mafanikio na mwelekeo wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kipindi cha miaka minne (4) ya Serikali ya Awamu wa Sita.
Dkt. Mafumiko amesema lengo la uwekezaji huo ni kuendelea kuimarisha uchunguzi wa kimaabara na kuendelea kutoa huduma bora za uchunguzi wa kisayansi wa kimaabara kwa wananchi kwa ufanisi zaidi.
AidhA, Dkt. Mafumiko ameeleza kuwa uchunguzi wa kisayansi wa kimaabara kwa sampuli umeongezeka kutoka sampuli 155,817 Mwaka Fedha 2021/2022 hadi kufikia sampuli 188,362 kwa mwaka wa Fedha 2023/2024, sawa na ongezeko la asilimia 21, na 2024/2025, kuanzia mwezi Julai hadi Desemba 2024, sampuli 108,851 zilifanyiwa uchunguzi sawa na asilimia 104.50 ya lengo la kuchunguza sampuli 104,161.
“Ongezeko la sampuli zinazochunguzwa na Mkemia Mkuu wa Serikali linatokana na kuongezeka kwa uelewa wa wananchi na wadau wa Mamlaka na ubora wa huduma za uchunguzi zinazotolewa na Mamlaka, pia ongezeko hili ni kutokana na ushirikiano na taasisi za Serikali za udhibiti kama vile Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulenya (DCEA), Jeshi la Polisi na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na wadau wa afya zikiwemo hospitali, OSHA (usalama mahali pa kazi) na NEMC (uchafuzi wa mazingira) na wadau wengine wanaotumia huduma za Mamlaka ili kupata uhakika wa ubora wa bidhaa zao,” ameeleza Dkt. Mafumiko.